kuza biashara yako

kuza biashara yako

Pages

Saturday, April 19, 2014

TUYAKEMEE MATUMIZI YA DAWA ZA KULEVYA KWA VIJANA

Dar es Salaam. Utumiaji wa dawa za kulevya umekuwa tatizo kubwa linaloikumba dunia hasa wakati huu wa utandawazi, huku sehemu ya waathirika wakuu wa dawa hizo wakiwa vijana ambao ni nguvukazi ya taifa.
Vijana wengi wanaotumia dawa za kulevya wamekuwa wakieleza chanzo kikuu cha wao kujiingiza katika matumizi hayo ni kushawishiwa na marafiki zao na ugumu wa maisha.
Hapa nchini vita ya dawa za kulevya imekuwa kubwa kadri siku zinavyozidi kusonga mbele huku wahusika wakuu wakielezwa kuwa ni vijana. Kundi hili ambalo ni nguvukazi ya taifa, wamekuwa wakitumika kusafirisha sehemu mbalimbali za dunia na nyakati zingine wao wenyewe wakitumia.
Mara kadhaa Serikali imekuwa ikitoa karipio kwa wahusika kwa kutangaza vita dhidi ya waagizaji, wasafirishaji na watumiaji ili kuhakikisha vita dhidi ya dawa za kulevya inatekelezwa kwa vitendo jambo ambalo halijafanikiwa.
Katika uwanja wetu wa sauti za vijana, tuliwauliza, Vijana mnaishauri nini Serikali kuhusu vita dhidi ya dawa za kulevya? Hivi ndivyo walivyosema: Mshana Joseph(35): Tatizo lililopo hapa ni wahusika wa dawa za kulevya ndiyo hao hao ambao wanatakiwa kusimamia na kutekeleza sheria mbalimbali, hivyo ni jambo ambalo haliwezekani endapo hakutakuwa na viongozi wenye uchungu na taifa lao kwani wataendelea kuliangamiza taifa.
Mohamend Juma(25): Serikali inatakiwa kutambua kuwa, waathirika wakuu ni sisi vijana hivyo itengeneze sheria kali kwa wahusika ambao watakuwa wanabainika kujihusisha na vitendo vya uagizaji na uuzaji, kwani bila kufanya hivyo ni dhahiri kwamba taifa litakosa viongozi wa baadaye wengi watakuwa ni waathirika wa dawa hizo.
Alexander Timbati (39): Tuna kila sababu ya kuilaumu Serikali kutokana na kufumbia macho watu ambao wamekuwa wakijihusisha na usambazaji wa dawa hizo, Serikali inawajua ila haiwachukulii hatua ni wakati sasa wa kufumbua macho na kuanza kuwashughulikia kwa masilahi ya taifa.
Asteria Kanangi: Asante kwa mada nzuri, mimi ninachokiona hapa ni kutokuwapo kwa usimamizi ipasavyo kwa sheria zinazohusika, Serikali iwachukulie hatua kali wale wote ambao wanahusika bila kujali cheo cha mtu na ikiwezekana wanyongwe kama China wanavyofanya.
David Samson (27): Tuna kila sababu ya kuilaumu Serikali kwa kushindwa kuwakamata wahusika, nimekuwa nikisikia bungeni wabunge wakisema wanawajua wahusika, lakini baada ya hapo hakuna chochote kinachoendelea, uzembe wa Serikali utakuja kuliweka njiapanda taifa kwa kuoneana haya na kulindana.

No comments :

Post a Comment